Ameeleza Ubada bin Swamiti radhi za Allah ziwe juu yake, na alikuwa ni miongoni mwa walioshuhudia vita vya Bardi kuu, naye akiwa kiongozi wa watu wake waliokuja kutoa mkono wa ahadi ya uaminifu kwa ajili ya kumnusuru Mtume rehema na amani ziwe juu yake usiku wa Aqaba ambayo iko Mina, wakati Mtume akiwa Makka kabla ya kuhama kwake kwenda Madina, ni kuwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake alikuwa kakaa na Maswahaba zake akawataka wamuahidi juu ya mambo haya: La kwanza: Wasishirikishe katika ibada za Mwenyezi Mungu kitu chochote hata kikiwa kidogo. La pili: Wasiibe. La tatu: Wasifanye uchafu wa zinaa. La nne: Wasiwauwe watoto wao; wa kiume kwa kuhofia ufakiri na umasikini au watoto wa kike kwa kuhofia fedheha. La tano: Wasilete uongo wataoutengeneza baina ya mikono yao na miguu yao, kwa sababu matendo mengi hutokea kupitia hivi viwili hata kama viungo vingine vitashiriki. La sita: Wasimuasi Mtume rehema na amani ziwe juu yake katika jambo jema. Atakayethubutu miongoni mwao katika ahadi na akashikamana nayo basi malipo yake yako kwa Mwenyezi Mungu, na atakayefanya lolote miongoni mwa hayo yaliyotajwa -kasoro ushirikina- akaadhibiwa katika dunia kwa kusimamishiwa adhabu juu yake basi hilo ndio kafara yake, na kwa hilo dhambi lake litaondoka, na atakayefanya lolote miongoni mwa hayo kisha Mwenyezi Mungu akamsitiri basi huyu jambo lake liko kwa Mwenyezi Mungu; akitaka atamsamehe na akitaka atamuadhibu, wote waliokuwepo wakampa ahadi ya utiifu juu ya hayo.