Anaamrisha Mtume -Rehema na amani ziwe juu yake- umma wake kujitenga mbali na maovu saba na maasi yenye kuangamiza, na alipoulizwa ni yapi hayo? akayabainisha kuwa ni: La kwanza: Ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kitu kingine, kwa kujifanyia mshirika na mfano wake utakasifu ni wake kwa namna yoyote ile itakayokuwa, na kuielekeza aina yoyote ya ibada miongoni mwa ibada kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kaanza na ushirikina; kwa sababu ndio dhambi kubwa kuliko yote. La pili: Uchawi -Nao namna ya ufungaji mafundo na makombe na madawa na ufukishaji mioshi-, yanayoleta athari katika mwili wa mwenye kurogwa kwa kuua au kutia maradhi, au kuwatenganisha kati ya wana ndoa wawili, nayo ni kazi ya kishetani, na wengi wao hawaufikii uchawi isipokuwa kwa ushirikina na kujikurubisha kwa maruhani wachafu kwa kitu wanachokipenda. La tatu: Ni kuua nafsi aliyokataza Allah isiuliwe isipokuwa kwa kigezo cha kisheria, na hutekelezwa na hakimu. La nne: Kutumia riba kwa kula au kwa njia nyingine katika njia za kunufaika. La tano: Kufanya uadui katika mali ya mtoto mdogo aliyefiwa na baba yake naye akiwa chini ya umri wa kubalehe. La sita: Kukimbia katika vita kati ya waislamu na makafiri. La saba: Kuwatuhumu wanawake huru wenye kujizuia na machafu kwa uzinifu, na vile vile kuwatuhumu wanaume.