Bedui mmoja anayeishi jangwani alimuuliza Mtume rehema na amani ziwe juu yake: Je, saa ya Kiyama itatokea wakati gani? Basi rehema na amani ziwe juu yake akamwambia: Umeiandalia mambo gani mema? Akasema muulizaji: Sikutayarisha jambo kubwa kwa ajili yake isipokuwa ninampenda Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na wala hakutaja ibada nyinginezo za moyo, za kimwili, au za kifedha. Kwa sababu zote ni matawi ya upendo unaotokana na hayo, na kwa sababu upendo wa dhati humsukuma mtu kujitahidi kufanya matendo mema. Mtume rehema na amani ziwe juu yake akamwambia: Wewe utakuwa pamoja na unayempenda peponi. Maswahaba wa Mtume rehema na amani ziwe juu yake wakafurahishwa sana na habari hii njema. Kisha Anas radhi za Allah ziwe juu yake akaeleza kuwa hakika anampenda Mtume rehema na amani ziwe juu yake na Abubakari na Omari, na anatarajia kuwa pamoja nao, hata kama amali zake si kama amali zao.