Anaeleza Mtume rehema na amani ziwe juu yake kuhusu fadhila za kuwahi kwenda kuswali swala ya Ijumaa mapema. Na kuwasili mapema kunaanza tangu kuchomoza jua hadi kuwasili kwa Imam; Nazo ni saa tano, na zinagawanywa katika sehemu tano kulingana na muda kati ya kuchomoza kwa jua mpaka kuingia kwa imamu na kupanda kwake juu ya mimbari kutoa hotuba. Ya kwanza: Atakayeoga josho kamili, kama kuoga janaba, kisha akaenda katika msikiti wa Ijumaa katika saa ya kwanza, ni kama katoa sadaka ya ngamia. Ya pili: Mwenye kwenda saa ya pili ni kama katoa sadaka ya ng'ombe. Ya tatu: Yeyote atakayekwenda saa ya tatu ni kama ametoa sadaka kondoo dume mwenye pembe. Ya nne: Mwenye kwenda katika saa ya nne ni kama ametoa sadaka kuku. Ya tano: Mwenye kwenda saa tano, ni kama ametoa yai katika sadaka. Anapotoka imamu kwenda kutoa hotuba; Malaika waliokaa milangoni huacha kuwaandikia thawabu wale wanaoingia msikitini mmoja mmoja, na huja kusikiliza ukumbusho na hotuba.