Mama wa Waumini Maimuna Mwenyezi Mungu amuwie radhi, alitueleza jinsi Mtume, Rehema na amani ziwe juu yake alivyokuwa akioga janaba, kiasi kwamba alimuwekea maji ya kuoga, na akamfunika kwa pazia, basi Mtume, Rehema na amani ziwe juu yake, akafanya yafuatayo: Kwanza: Alimimina maji kwenye mikono yake na akaiosha kabla ya kuiingiza katika chombo. Pili: Alimimina maji kwa mkono wake wa kulia juu ya mkono wake wa kushoto na kuosha sehemu zake za siri ili kuisafisha kutokana na athari yoyote ya janaba. Tatu: Aliipiga ardhi kwa mkono wake, akaufuta, kisha akauosha ili kuondoa udhia. Nne: Alisukutukua; Kwa kuingiza maji katika kinywa chake na kuyazungusha, kisha kuyatema; na akavuta maji puani kwa pumzi yake, kisha akayatoa nje ili kuisafisha. Tano: Aliosha uso wake na mikono yake. Sita: Alimimina maji juu ya kichwa chake. Saba: Alimimina maji katika mwili wake mzima. Nane: Alitoka mahali alipoogea na akaosha miguu yake katika mahali pengine, kwani hakuiosha mwanzo. Kisha akamletea kitambaa ili ajifute kwacho, akawa hakukichukua, na akaanza kufuta maji kutoka mwilini kwake kwa mkono wake, na anayapangusa.